Saturday, July 27, 2024

Jifunze, Chukua Hatua Kuboresha Afya Yako

Afya

FAHAMU TATIZO LA SARATANI YA KOO NA MATIBABU YAKE.

Saratani ya kooni ni aina ya saratani inayoshambulia njia yako ya chakula ambayo husafirisha chakula kwanzia mdomoni mpaka tumboni, ugonjwa huu huanzia ndani ya koo kisha kusambaa sehemu mbalimbali za mwili.

Saratani ya koo ni ya sita duniani kwa kusababisha vifo na wahanga wengi wa ugonjwa huu ni wanaume kuliko wanawake..Nchini Tanzania wagonjwa hawa wapo wengi hasa kwenye hospitali kubwa za rufaa lakini waathirika wakubwa ni watu wazima kwanzia Miaka 50 kwenda mbele.

Nini chanzo cha ugonjwa huu?

Kama ilivyo kwa aina zote za saratani duniani mara nyingi chanzo halisi hua hakifahamiki mambo hatarishi ambayo huchangia kuanza kwa ugonjwa huu kama ifuatavyo.

kuvuta sigara
unywaji wa pombe kupitiliza.
kiungulia cha muda mrefu
unene
kula vyakula vya moto sana
kutokula matunda na mboga za majani.
magonjwa mengine ya koo mfano achalasia.
dalili za saratani ya koo
kushindwa kumeza chakula; mara nyingi mgonjwa huanza na kushindwa kumeza chakula kigumu kama ugali, baadae hushindwa uji, kisha hushindwa maji ya kunywa na mwisho kabisa hushindwa kabisa hata kumeza mate.
kukohoa na sauti kukoroma; dalili hii mara nyingi hutokea mwishoni kwani koo linakua limetoboka na chakula kinaingia kwenye njia ya hewa lakini pia mishipa ya fahamu ya sauti inakua imeingiliwa na saratani
kupungua uzito sana.
maumivu ya kifua.
kiungulia kikali.
jinsi ya kutambua ugonjwa.
Kipimo cha endoscopy au OGD ambacho kina mpira wenye camera maalumu hupitishwa kooni mpaka tumboni kuangalia saratani hiyo lakini pia kipimo hiko hiko hutumika kutoa nyama kitaalamu kama biopsy na kwenda kupima maabara.
Vipimo vingine kama PET scan,CT scan na broncoscopy hufanyika kuangalia ugonjwa umesambaa kiasi gani.

Matibabu ya saratani ya koo.
Matibabu ya ugonjwa huu hutegemea na hatua ya ugonjwa husika, katika hatua ya kwanza mpaka ya tatu ya ugonjwa ambayo ugonjwa unakua bado uko ndani ya koo upasuaji huweza kufanyika kuondoa vimbe za saratani hizo kitaalamu kama oesophagectomy lakini ugonjwa ukishasambaa kwenye hatua ya nne ya ugonjwa basi panakua hapawezekani tena kupasua, mgonjwa anaweza kutumia dawa za saratani kama chemotherapy kuongeza muda wa kuishi.

maisha baada ya saratani.
Ugonjwa huu ukiwahiwa unaweza kutibiwa kabisa kwa upasuaji na kupona lakini kwenye hatua za mwisho mgonjwa atapewa tu ushauri na kupewa dawa za kupunguza maumivu ili aendelee kuishi muda uliobaki bila maumivu lakini pia atawekewa koo bandia ambalo litamsaidia kula kama alikua amefika hatua ambayo hawezi kula tena.
Uwezekano wa kuishi miaka zaidi ya miaka mitano kwa saratani kwanzia steji ya kwanza mpaka ya 3 yaani inakua bado iko kwenye koo ni asilimia 47%, ikisambaa sehemu za pembeni ya koo kma kwenye mishipa ya damu na sehemu za kifua ni asilimia 25% lakini ikisambaa mwili mzima ni asilimia 5% tu.
Ni vizuri ndugu na mgonjwa kukubali ukweli mapema kuliko kutumia pesa nyingi kwa waganga wa kienyeji au hata kwenda nje ya nchi kwani hakuna faida yeyote ya kufanya hivo.

STAY ALIVE

 

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *